Banner

Banner

Thursday, February 27, 2025

WAFUNGWA 118 KUNUFAIKA NA MPANGO WA PAROLE


Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Parole  Mhe. Balozi Khamis Kagasheki Feberuari 20, 2025 aliongoza kikao cha 52 cha  Bodi ya Taifa ya Parole kilichofanyika kwa muda wa siku mbili katika Ukumbi wa Corridor Springs Hotel jijini Arusha ambapo 
wajumbe wamejadili na kupendekeza wafungwa ambao wana sifa ya kunufaika na mpango wa Sheria ya Parole.

Pia Mhe. Kagasheki alisema kuwa wafungwa waliojadiliwa wameshatumikia sehemu ya kifungo chao gerezani na kifungo kilichobaki wataenda kumalizia wakiwa na familia zao na jamii kama Sheria ya Parole inavyotaka.

''Bodi imepitia kwa umakini majalada 132 na kuona kama vigezo, Kanuni, taratibu na Sheria zimefuatwa  hivyo basi Bodi imeamua kuwa wafungwa 118 wanastahili kunufaika na mpango huo wa Parole'' Alisema Kagasheki.

Kwa upande wake Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Jeremiah Yoram Katungu ametoa rai kwa jamii na wananchi kwa ujumla kushirikiana kwa pamoja na Jeshi la Magereza kuwapokea Wafungwa ambao wanatarajia kutoka gerezani kwa mpango wa Parole, nakusema kuwa Wafungwa hawa wamejirekebisha kitabia na mienendo yao wakiwa gerezani.

Pamoja na mambo mengine CGP Katungu alisema kuwa utaratibu wa Parole umewekwa kwa mujibu wa Sheria na umeainisha vigezo ambavyo vinatakiwa kuzingatiwa ili mfungwa aweze kunufaika na mpango huo, akivitaja vigezo hivyo ikiwemo urefu wa kifungo chake, tabia na mwenendo wake akiwa gerezani, lakini kama jamii nayo iko tayari kumpokea, hayo yote yanazingatiwa wakati Bodi inamjadili mfungwa huyo ili aweze kupendekezwa kwa utaratibu wa Parole.

Kikao hicho cha 52 cha Bodi ya Taifa ya Parole kimejadili jumla ya majalada 132, na majalada 118 yamekidhi vigezo vya mpango huo.

WAZIRI BASHUNGWA AZINDUA MABASI YA KUSAFIRISHA MAHABUSU KWENDA NA KURUDI MAHAKAMANI

 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Innocent Lugha Bashungwa, Februari 14, 2025 alifanya ziara Makao Makuu ya Jeshi la Magereza na kuzindua Mabasi Saba ya kubebea Mahabusu kwenda na kurudi Mahakamani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mabasi hayo Mhe. Bashungwa amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri na kubwa anayo endelea kuifanya ya kuboresha Jeshi la Magere

za kwa kulipatia vifaa na vitendea kazi mbalimbali ikiwemo mabasi tuliyo yazindua na kutoa wito wa kuyatunza magari hayo ili yadumu na kutoa huduma iliyokusudiwa.

"Nitumie nafasi hii kumshukuru sana Rais wetu na Amiri Jeshi Mkuu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanya yakuboresha Jeshi letu la Magereza, kuliwezesha Jeshi letu la Magereza kuwa na vifaa na vitendea kazi kama ambavyo tumeshuhudia uzinduzi wa mabasi haya ambayo yanaenda kuboresha huduma kwa ndugu zetu wafungwa" alisema Mhe. Bashungwa

Aidha,  Mhe. Bashungwa amelipongeza Jeshi la Magereza nchini kwa kutekeleza kikamilifu jukumu la kuwapa ujuzi wafungwa ikiwemo ufundi stadi na kuuendeleza ujuzi wa wafungwa wanaoingia nao, huku akieleza mkakati uliopo wa kuzindua program maalum kwa kushirikiana na VETA ili kutoa vyeti kwa wafungwa baada ya kupata ujuzi Gerezani.

Katika hatua nyingine Mhe. Bashungwa amempongeza CGP. Katungu kwa kusimamia agizo la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, la kuachana na matumizi ya kuni na kuanza kutumia nishati safi ya kupikia katika Magereza yote hapa nchini.

Monday, November 25, 2024

CGP. KATUNGU AFANYA KIKAO NA WAKUU WA MAGEREZA YOTE TANZANIA BARA

Mkuu wa Jeshi la Magereza Nchini (CGP  Yoram Katungu Novemba 23, 2024 alifanya kikao kazi na wakuu wa Magereza  Mikoa yote Tanzania bara na kuwataka wakuu hao kutokuwa na makundi, mivutano na migongano mahala pa kazi na kuhimiza Umoja, Ushirikiano na Upendo ili kuwa na mwelekeo mmoja kama Jeshi.


CGP. Katungu, alisisitiza masuala mbalimbali ya kiutendaji ikiwemo programu za mfungwa anapoingia gerezani afanyiwe tathmini ya kina ili kugundua uwezo wake na kumpangia program ya  kumfaa katika kufanikisha suala la Urekebishaji kwa mfungwa husika na pindi anapokaribia kumaliza kifungo chake, aandaliwe kisaikolojia namna bora ya kwenda kuishi na jamii ukizingatia kwasasa Jeshi linafanya  mapitio ya Sheria ya kuwafuatilia wafungwa pindi wanapokuwa wamemaliza vifungo vyao.

Kwa upande wake Mkuu wa Divisheni ya Fedha na Mipango Kaimu Kamishna wa Magereza (DCP) Chacha Bina, alipongeza wakuu wa Magereza kwa jitihada zao za kuhakikisha maduhuli ya serikali yanapatikana kwa wakati na kuvuka malengo ya kukusanya maduhuli hayo akisisitiza kuwa maduhuli si takwa la Mkuu wa Jeshi, bali ni agizo la Serikali.


Katika kikao kazi hicho wakuu wa Divisheni, Vitengo na Sehemu waliwasilisha mada mbalimbali.