Mojawapo ya Jukumu la Jeshi la Magereza ni kuwapeleka mahakamani mahabusu na kuwarudisha magerezani.

Gadi ya askari Wanawake na Wanaume wa Jeshi la Magereza katika Maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa.

Ng'ombe bora wa Nyama na Maziwa ni sehemu ya miradi ya Uzalishaji inayoendeshwa na kusimamiwa na Jeshi la Magereza nchini.

Sehemu ya Mashamba makubwa yanayoendeshwa na Jeshi la Magereza: Shughuli za Kilimo cha Mashamba makubwa, madogo na bustani za mboga mboga ni moja ya shughuli za Magereza katika kuwafunza wafungwa namna ya kujitegemea mara wamalizapo vifungo vyao.

Baadhi wa wafungwa katika Kiwanda cha Ushonaji nguo cha Gereza Kuu Ukonga wakiwa kazini: Shughuli za Ushonaji wa nguo ni moja ya eneo ambalo wafungwa hupata huduma za urekebishwaji kwa vitendo.

Sunday, November 18, 2018

KATIBU MKUU WA MAMBO YA NDANI, MEJA JENERALI JACOB KINGU AKAGUA MABORESHO YA KIWANDA CHA VIATU GEREZA KUU KARANGA MOSHI

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani, Meja Jenerali Jacob Kingu akisalimiana na Maafisa wa Jeshi la Magereza Mkoani Kilimanjaro mara baada ya kuwasili katika ziara Maalum ya kukagua maboresho mbalimbali katika Kiwanda cha Viatu cha Gereza Kuu Karanga Moshi jana  Novemba 17, 2018. Kushoto kwake ni Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu(meza kuu) akitoa maelekezo kwa Kaimu Mkuu wa Kiwanda hicho, Mrakibu Msaidizi wa Magereza, Hamis Nyaku(aliyesimama). Kushoto ni Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu na Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike wakiangalia Buti za aina mbalimbali za Jeshi zinazotengenezwa katika Kiwanda cha Viatu Karanga Moshi.
Sehemu ya viatu aina mbalimbali ikiwemo viatu vya maafisa na Buti za Jeshi zinazotengenezwa katika Kiwanda cha Viatu Karanga Moshi kwa ajili ya Jeshi la Polisi nchini. Jeshi la Polisi limetengenezewa viatu aina ya buti pea elfu kumi (10,000) na pea elfu tano (5,000) za viatu vya maafisa zenye thamani ya Tsh. 1, 237, 666, 600/=, tayari buti zimekabidhiwa kwa Jeshi hilo na hivi sasa kiwanda kinamalizia utengenezaji wa viatu vya maafisa wa Jeshi la Polisi.

Maafisa Masoko wa Kiwanda cha viatu Karanga Moshi wakivipanga viatu vya kiraia aina mbalimbali vinavyotengenezwa katika kiwanda hicho kama inavyoonekana katika picha.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu akipata maelezo ya kitaalam juu ya utengenezaji wa Buti za Jeshi kutoka kwa Mtaalam wa utengenezaji viatu wa Jeshi la Magereza
(Picha zote na Jeshi la Magereza).

KATIBU MKUU MAMBO YA NDANI NA CGP KASIKE WATEMBELEA KIWANDA CHA SAMANI CHA JESHI LA MAGEREZA CHA ARUSHA KILICHOTEKETEA KWA MOTO


Na Lucas Mboje, Arusha
KATIBU Mkuu Wizara ya Mambo ya  Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu pamoja na Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike leo wametembelea Kiwanda cha Samani cha Arusha, mali ya Jeshi la Magereza ili kujionea athari mbalimbali iliyosababishwa na ajali ya moto iliyotokea juzi Novemba 16, 2018.
Akizungumza eneo la tukio Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu amesema kuwa ni vyema taasisi mbalimbali nchini pamoja na wananchi wakachukua tahadhali za majanga ya moto ili kuepusha hasara zinazoweza kujitokeza kufuatia majanga hayo.
Amesema kuwa Wizara yake itaendelea kuliwezesha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji vifaa vya kisasa ili liweze kukabiliana na majanga ya moto pindi yanapojitokeza.
Aidha, Katibu Mkuu huyo, Meja Jenerali Kingu amelitaka Jeshi la Magereza kuhakikisha kuwa linafanya jitihada za haraka za kurejesha shughuli za uzalishaji katika kiwanda hicho ikiwemo kufanyia matengenezo baadhi  ya mashine zilizoteketezwa na moto.
Kwa upande wake, Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike amevishukru vyombo vya ulinzi na usalama ikiwemo Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na Jeshi la Polisi Mkoani Arusha sambamba na wananchi waliojitokeza kusaidia katika uzimaji wa moto huo ambao umeunguza sehemu ya kiwanda hicho.
“Nawashukru sana Jeshi la zimamoto na uokoaji Mkoani Arusha, Jeshi la Polisi pamoja na wananchi kwa kazi kubwa waliyoifanya siku ya tukio kwani niliarifiwa kuwa moto ulikuwa mkubwa lakini tunashukuru Mungu hatimaye uzimaji ulifanikiwa pamoja na hasara iliyojitokeza”. Alisema Jenerali Kasike.
Akizungumzia chanzo cha moto huo na hasara iliyojitokeza, Kamishna Jenerali Kasike amesema kuwa taarifa za awali zinaonesha kuwa moto huo ulisababishwa na hitilafu ya umeme ambayo ilisababisha kuteketea kwa baadhi ya mashine za kiwanda hicho pamoja na uharibu wa nyaraka mbalimbali za ofisi katika jengo la utawala.
Wakati huo huo, Kamishna Jenerali Phaustine Kasike ameunda Kamati maalum ya Maafisa watano kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Magereza ambayo itachunguza chanzo cha moto huo pamoja na kuwasilisha taarifa kamili ya hasara iliyojitokeza. Tume hiyo itaongozwa na Kamishna wa Fedha na Mipango wa Jeshi hilo, Kamishna wa Magereza, Gideon Nkana.
Kiwanda cha samani cha Magereza Arusha kilimikishwa rasmi kwa Jeshi la Magereza mwaka 1973 baada ya Azimio la Arusha mwaka 1967 ambapo tangu kipindi hicho kiwanda hicho kinajishughulisha na utengenezaji wa samani mbalimbali za ofisi na samani za majumbani. Pia kiwanda hiki hutumika kuwafundisha na kuwarekebisha wafungwa ili wamalizapo vifungo vyao waweze kujitegemea kupitia ujuzi waliojifunza.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu akiwasili Novemba 17, 2018 katika Kiwanda cha samani cha Magereza Arusha kukagua sehemu mbalimbali ambazo moto umeteketeza sehemu ya kiwanda hicho. Kushoto kwake ni Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike.

Mkuu wa Magereza Mkoa huo, ACP Anderson Kamtiaro akisoma taarifa ya janga la moto mbele ya Katibu Mkuu Mambo ya ndani ya nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu aliwasili kiwandani kujionea uhabribu mbalimbali uliojitokeza.

Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike akitoa taarifa kwa Katibu Mkuu Mambo ya ndani ya nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu kuhusu hatua mbalimbali ambazo amezichukua ikiwemo kuunda kamati maalum ya watu watano ambayo itachunguza tukio la moto katika kiwanda hicho.

Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike (wa pili toka kulia) pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu (kulia kwake), wakiangalia moja ya mashine mbalimbali ambazo zimeteketezwa na moto katika kiwanda cha Samani cha Magereza Arusha. Chanzo cha moto huo inasemekana ni hitilafu ya umeme ndani ya kiwanda hicho.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu (wa kwanza kushoto) akitoa maelekezo mbalimbali kwa Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike(katikati). Kulia ni Kamishna wa Fedha na Mipango, Kamishna wa Magereza, Gideon Nkana ambaye ni Kiongozi wa Kamati Maalum ya kuchunguza tukio hilo.

Jengo la kiwanda cha samani cha Magereza Arusha ambalo limeteketea kwa moto.

Muonekano wa baadhi ya mashine pamoja na vifaa mbalimbali na nyaraka nyinginezo za ofisi zilizoungua kufuatia janga la moto.

Samani mbalimbali zinazotengenezwa katika kiwanda cha samani cha Magereza Arusha kama inavyoonekana katika picha zikiwa tayari kwenda sokoni(Picha na Jeshi la Magereza).

Friday, November 16, 2018

MKUU WA JESHI LA MAGEREZA AKUTANA NA RC NJOMBE KABLA YA KUHITIMISHA ZIARA YAKE TAREHE 15/11/2018

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Christopher Ole Sendeka akisalimiana na Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Phaustine Kasike  alipotembelea Ofisi za Mkuu wa Mkoa kabla ya kuhitimisha ziara yake ya kikazi, Novemba 15, 2018.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Christopher Ole Sendeka akitoa taarifa fupi ya Mkoa wake alipotembelewa na Mkuu wa Jeshi la Magereza Ofsini kwake.
Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike akielezea malengo ya ziara yake ya kikazi mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Njombe alipotembelea Ofisi za Mkoa huo.


Mkuu wa Jeshi la Magereza, CGP. Phaustine Kasike akiagana na baadhi ya askari wa Gereza Njombe baada ya kuhitimisha ziara yake ya kikazi Mkoani Njombe.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Christopher Ole Sendeka (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na  Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike(wa pili toka kulia) pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Njombe. Wa pili toka kushoto ni Katibu Tawala Mkoa wa Njombe, Bw. Erick Shitindi ( Picha na Jeshi la Magereza).

Thursday, November 15, 2018

ZIARA YA CGP KASIKE GEREZA LA WILAYA MAKETE, MKOANI JOMBE



Mkuu wa Jeshi la Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike akizungumza jambo alipotembelea Ofisi za Mkuu wa Wilaya Makete Novemba 14, 2018. Wengine ni Maafisa Waandamizi wa Jeshi hilo.
Baadhi ya Askari wa kike wa Jeshi la Magereza wakiteta jambo na Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike ambapo askari hao wamempongeza Mkuu wa Jeshi hilo kwa uamuzi wake wa kutembelea magereza mbalimbali hapa nchini.
Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Phaustine Kasike akiwasili Gereza Makete tayari kwa ziara yake ya kikazi Mkoani Njombe, Novemba 14,  2018.

 Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike akikagua maandalizi ya mashamba ya kilimo cha mahindi katika eneo la Gereza Ludewa mapema leo asbuhi Novemba 14, 2018  kabla ya kuelekea Gereza Makete kuendelea na ziara yake ya kikazi.
Mkuu wa Gereza Makete, SP. Aloyce Kayera(kushoto) akisoma taarifa ya Gereza mbele ya Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike(kulia) alipotembelea gereza hilo leo Novemba 14, 2018.
. Mkuu wa Wilaya ya Makete, Mhe. Veronica Kessy akiagana na Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike alipotembelea Ofisi za Mkuu wa Wilaya Makete.


Wednesday, November 14, 2018

GEREZA LUDEWA KUPATIWA TREKTA ILI KUONGEZA UZALISHAJI WA CHAKULA CHA WAFUNGWA


Na Lucas Mboje, Ludewa

KAMISHNA Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike ameahidi kulipatia trekta moja Gereza la Kilimo Ludewa ili kuongeza uzalishaji wa chakula cha wafungwa.

Kamishna Jenerali Kasike ametoa ahadi hiyo leo wakati akizungumza na uongozi wa Gereza hilo baada ya kuwasili Wilayani Ludewa katika ziara yake ya kikazi ya kukagua utendaji kazi wa Jeshi hilo.

Amesema kuwa Gereza Ludewa ni miongoni mwa magereza 13 ambayo tayari yameainishwa katika mpango mkakati wa Jeshi la Magereza katika kujitosheleza kwa chakula cha wafungwa waliopo magerezani hivyo lazima liwezeshwe zana za kilimo.

 “Nafahamu kuwa trekta lililopo hapa Gereza Ludewa ni la muda mrefu na ni chakavu, hivyo nitawapatieni trekta jipya ili muweze kuongeza uzalishaji wa chakula cha wafungwa”. Alisema Jenerali Kasike.

Pia, Kamishna Jenerali Kasike amehimiza uongozi wa Gereza hilo kuzingatia suala zima la uadilifu na amewataka kujiepushe na vitendo vyote vya ubadhilifu wa mali za umma.

Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza hilo, SSP. Akley Mkude amesema kuwa  katika msimu wa Kilimo wa mwaka 2017/2018 gereza hilo lililima ekari 200 za mahindi na kufanikiwa kuvuna gunia zaidi ya 1700 ambazo zitatumika kulisha magereza yote ya Mkoa wa Njombe na Iringa.

Aidha, ameongeza kuwa  malengo ya msimu huu wa mwaka 2018/2019 ni kulima ekari 700 za mahindi, ekari 40 za maharage, ekari 30 za alizaeti pamoja na bustani ekari 5 za mbogamboga.

Gereza Ludewa lina eneo lenye ukubwa wa ekari 3500, Gereza hilo linajishughulisha na kilimo cha mahindi, maharage, alizeti pamoja na bustani za mbogamboga. Pia, linajishughulisha na miradi ya ufugaji wa ng’ombe, mbuzi, kuku wa kienyeji pamoja na uhifadhi wa mazingira.


Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Phaustine Kasike akisalimiana na Maofisa na askari wa Gereza Ludewa alipowasili kuendelea na ziara yake ya kikazi ya kutembelea magereza mbalimbali Mkoani Njombe,  Novemba 13, 2018.

Mkuu wa Gereza Ludewa, SSP. Akley Mkude(kushoto) akimweleza jambo Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike(kulia) alipotembelea gereza hilo  Novemba 13, 2018. Wengine ni Maafisa Waandamizi wa Jeshi hilo.

Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike akipanda mti wa mparachichi katika Kambi ya Jeshi la Magereza ya Kidewa iliyopo Mkoani Njombe kabla ya kuendelea na ziara yake ya kikazi Gereza Ludewa, Novemba 13, 2018.
Ghala la kuhifadhia mahindi yanayozalishwa katika Gereza Ludewa.

Baadhi ya Askari wa Gereza la Wilaya Ludewa  wakimsikiliza Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike(hayupo pichani).

Mkuu wa Wilaya ya Ludewa, Mhe. Andrea Tsere(wa tatu toka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike(wa pili toka kulia) pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilayani Ludewa( Picha na Jeshi la Magereza).

Monday, November 12, 2018

WAKUU WA MAGEREZA NCHINI WATAKIWA KUWA WABUNIFU KATIKA UTATUZI WA NYUMBA ZA ASKARI


Na Lucas Mboje, Njombe

WAKUU wa Magereza yote nchini wametakiwa kuwa wabunifu ili kutatua changamoto ya uhaba wa makazi ya askari kwa kutumia nguvukazi ya wafungwa na rasilimali nyinginezo zilizopo katika maeneo yao.

Wito huo umetolewa leo Novemba 12, 2018 na Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike alipofanya ziara ya kikazi ya kukagua magereza yote ya Mkoa wa Njombe ambayo yanaendeshwa na Jeshi hilo.

Kamishna Jenerali Kasike amesema kuwa lazima wakuu wa magereza wawe wabunifu katika kutatua tatizo hilo la uhaba wa nyumba kwani Jeshi hilo linazo fursa nyingi ikiwemo nguvu kazi ya wafungwa.

“Mkoa wa Njombe na mingineyo nchini haipo sababu ya kuwa na tatizo la uhaba wa nyumba za askari kwani kuna fursa ya kutosha ya kufyatua tofali za kuchoma  kwa kuwatumia wafungwa ili kumaliza tatizo hili nchini”. Amesisitiza Jenerali Kasike.

Aidha, Kamishna Jenerali Kasike amewataka mafisa na askari wote kuendelea kutimiza majukumu yao kwa kuzingatia maadili, sheria na kanuni mbalimbali za uendeshaji wa Jeshi hilo.

Awali, akisoma taarifa ya Gereza la Wilaya Njombe, Mkuu wa Gereza hilo, SP. Charls Mihinga amesema kuwa  tayari wameanzisha mradi wa ufyatuaji wa tofali za kuchoma katika kambi ya mdandu ili kumaliza tatizo la uhaba wa nyumba za watumishi wa gereza hilo.

“Katika msimu huu tumeweza kufyatua tofali kubwa zipatazo 30,000 ambazo tayari zimeshachomwa, tofali hizi zitatumika katika ujenzi wa nyumba za askari pamoja na ujenzi wa Ofisi mpya ya Mkuu wa Magereza Mkoani Njombe”. Alisema SP. Mihinga.

Pia, ameongeza kuwa  malengo ya baadaye ni kuifanya kambi hiyo ya Gereza Njombe kuwa na taswira ya uzalishaji wa matofali kwa wingi kwa ajili ya kufanya biashara na hivyo kuongeza maduhuri serikalini.

Jeshi la Magereza linakabiliwa na uhaba wa nyumba za kuishi za Maafisa na askari hapa nchini, mkakati uliopo hivi sasa chini ya uongozi wa Kamishna Jenerali wa Magereza ni kuhakikisha kuwa tatizo hilo linatatulika kwa kutumia njia ya ubunifu pamoja na fursa mbalimbali zilizopo ndani ya Jeshi hilo.
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Njombe ambaye pia ni Katibu Tawala wa Mkoani Njombe Bw. Erick Shitindi akisalimiana na Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Phaustine Kasike walipokutana  Mkoani Njombe alipotembelea Ofisi za Mkuu wa Mkoa huo kabla ya kuendelea na ziara yake ya kikazi Mkoani Njombe, leo Novemba 12,  2018.

Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Njombe wakimsikiliza  Mkuu wa Jeshi la Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike(hayupo pichani) alipotembelea Ofisi za Mkuu wa Mkoa kabla ya kuendelea na ziara yake ya kikazi Mkoani humo.
Baadhi ya Askari wa Gereza la Wilaya Njombe  wakifuatilia maelekezo katika Baraza lililoongozwa na  Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike ambapo askari hao wameelezea changamoto zao kiutendaji leo Novemba 12, 2018.
Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike(katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Maafisa na askari wa Gereza Njombe.

Mkuu wa Jeshi la Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike(wa kwanza kulia) akizungumza jambo alipotembelea Ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Njombe. Wengine ni Maafisa Waandamizi wa Jeshi hilo.

Mkuu wa Gereza Njombe, SP. Charles Mihinga(kushoto) akimtembeza Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike(kulia) alipotembelea gereza hilo leo Novemba 12, 2018.( Picha na Jeshi la Magereza)

Friday, November 9, 2018

KAMISHNA JENERALI WA MAGEREZA AASA JAMII KUACHA KUTENDA UHALIFU ILI KUPUNGUZA MSONGAMANO MAGEREZANI


Na Lucas Mboje, Iringa;

KAMISHNA Jenerali wa Jeshi la Magereza Magereza nchini, Phaustine Kasike ametoa rai kuwa ili kupunguza msongamano magerezani ni vema jamii ikaacha kufanya matukio mbalimbali ya uhalifu hapa nchini.

Rai hiyo imetolewa leo na Kamishna Jenerali Kasike wakati akitoa ufafanuzi mbele ya wanahabari wa Mkoani Iringa kuhusu madai ya uwepo wa msongamano wa wafungwa katika magereza mbalimbali yaliyopo nchini ambapo ameeleza kuwa si kweli kwamba magereza yote yana msongamano bali msongamano uliopo magerezani ni kwenye baadhi ya magereza yenye kuhifadhi mahabusu.

Amesema suala la msongamano limekuwa ni tatizo kubwa ambapo takwimu za Jeshi la Magereza zinaonesha kuwa idadi ya mahabusu waliopo magerezani ni wengi na hali hiyo inatokana na wingi wa matukio ya uhalifu kwenye eneo husika na kule ambako hakuna uhalifu mwingi basi nako kwenye magereza hakuna msongamano mkubwa wa wafungwa/mahabusu.

Ameongeza kuwa Jeshi la Magereza litaendelea kushirikiana na vyombo vya haki jinai ikiwemo Jeshi la Polisi, Mahakama na Ofisi ya DPP ili kuhakikisha kuwa kunakuwa na usukumaji wa kesi mbalimbali za mahabusu waliopo magerezani.

“Tutajitahidi kuendelea kushirikiana kwa pamoja katika jukwaa letu la haki jinai ili kuangalia namna bora zaidi ya kuweza kutatua tatizo la ucheleweshaji wa kesi za mahabusu waliopo magerezani”. Amesema Jenerali Kasike.

Kuhusu uhamisho wa Gereza Iringa kwenda eneo la la Mlolo, Kamishna Jenerali Kasike amesema tayari Jeshi hilo limekwishaanza kutekeleza maelekezo ya Serikali ambapo hivi sasa lipo katika mchakato wa kuhamishwa kadri hali ya kibajeti itakavyoruhusu.

“Tumekwishaanza ufyatuaji wa tofali za ujenzi wa nyumba za maafisa na askari sambamba na ujenzi wa mabweni ya wafungwa unaendelea katika eneo hilo hivyo Gereza Iringa litahamishiwa katika eneo la Mlolo ili kupisha huduma za kijamii”. Amesisitiza Jenerali Kasike.

Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini, CGP. Phaustine Kasike yupo mkoani Iringa  kwa ziara ya kikazi ambapo leo ametembelea magereza ya Iringa na Pawaga. Ziara hizi ni mwendelezo wa ziara zake  za kikazi zenye lengo la kukagua magereza yote Tanzania Bara na kuzungumza na Maafisa na askari pamoja na kujua changamoto mbalimbali wanazokutana nazo wakati wakitekeleza majukumu yao.
Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike akiwasili katika Gereza la Iringa leo Novemba 9, 2018 tayari kwa ziara yake ya kikazi yenye lengo la kukagua shughuli mbalimbali za uendeshaji wa Jeshi hilo.

Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike akikagua moja la ghala la kuhifadhia mpunga unaozalishwa katika Gereza la Kilimo Pawaga.

. Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike akizungumza na Mahabusu na Wafungwa wa Gereza Iringa(hawapo pichani) alipofanya ziara ya kikazi leo Novemba 9, 2018.

Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike akikagua maandalizi ya shamba ya kilimo cha mpunga katika eneo la Gereza la Pawaga Mkoani Iringa. Gereza Pawaga limepewa malengo ya kulima ekari 375 za mpunga ili kuwezesha mpango wa kujitosheleza kwa chakula cha wafungwa.

Mkuu wa Magereza Mkoa wa Iringa, Kamishna Msaidizi wa Magereza, Hassan Mkwanda akimuongoza Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike kutembelea maeneo mbalimbali ya Gereza la Wilaya Iringa.

Askari wa vyeo mbalimbali wa Gereza Pawaga wakifuatilia kwa makini maelekezo ya Kamishna Jenerali wa Magereza alipotembelea gereza hilo leo Novemba 9, 2018.

Kitalu cha mbegu za mpunga ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Kilimo mpunga katika eneo la Gereza la Pawaga Mkoani Iringa. Gereza Pawaga limepewa malengo ya kulima ekari 375 za mpunga ili kuwezesha mpango wa kujitosheleza kwa chakula cha wafungwa. (Picha na Jeshi la Magereza).

MKUU WA JESHI LA MAGEREZA NCHINI, CGP PHAUSTINE KASIKE AANZA ZIARA YA KIKAZI MKOANI IRINGA

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Iringa Mjini, Mhe. Richard Kasesela akisalimiana na Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Phaustine Kasike walipokutana  Mkoani Iringa alipotembelea Ofisi za Mkuu wa Mkoa kabla ya kuendelea na ziara yake ya kikazi, leo Novemba 8, 2018.

   Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Iringa Mjini, Mhe. Richard  Kasesela(watatu toka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na  Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike(wa tatu toka kulia) pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Iringa.


Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Phaustine Kasike (kushoto) akizungumza na Mkuu wa Magereza Mkoa wa Iringa,  Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Hassan Mkwanda na Maafisa wengine wa Magereza Mkoani Iringa, muda mfupi alipowasili leo Novemba 8, 2018 Mkoani humo. CGP Kasike yupo mkoani humo kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kukagua magereza yote ya Mkoa wa Iringa na kuzungumza na Maafisa na askari pamoja na kujua chamgamoto mbalimbali wanazokutana nazo wakati wakitekeleza majukumu yao.
Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Iringa wakisalimiana na Mkuu wa Jeshi la Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike walipokutana  Mkoani Iringa alipotembelea Ofisi za Mkuu wa Mkoa kabla ya kuendelea na ziara yake ya kikazi.
Baadhi ya Askari wa Gereza la Wilaya Iringa wakifuatilia maelekezo katika Baraza lililoongozwa na  Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike ambapo askari hao wameelezea changamoto zao kiutendaji leo Novemba 8, 2018.
Mkuu wa Magereza Mkoa wa Iringa,  Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Hassan Mkwanda  akimkaribisha Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini (CGP) Phaustine Kasike(katikati meza kuu) ili azungumze na baadhi ya Maafisa na askari wa Gereza Iringa(hawapo pichani, leo Novemba 8, 2018 . Kulia ni  ACP. Josephine Semwenda ambaye hivi karibuni ameteuliwa kuwa Mkuu wa Magereza Mkoa  wa Lindi ( Picha na Jeshi la Magereza).