Mojawapo ya Jukumu la Jeshi la Magereza ni kuwapeleka mahakamani mahabusu na kuwarudisha magerezani.

Gadi ya askari Wanawake na Wanaume wa Jeshi la Magereza katika Maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa.

Ng'ombe bora wa Nyama na Maziwa ni sehemu ya miradi ya Uzalishaji inayoendeshwa na kusimamiwa na Jeshi la Magereza nchini.

Sehemu ya Mashamba makubwa yanayoendeshwa na Jeshi la Magereza: Shughuli za Kilimo cha Mashamba makubwa, madogo na bustani za mboga mboga ni moja ya shughuli za Magereza katika kuwafunza wafungwa namna ya kujitegemea mara wamalizapo vifungo vyao.

Baadhi wa wafungwa katika Kiwanda cha Ushonaji nguo cha Gereza Kuu Ukonga wakiwa kazini: Shughuli za Ushonaji wa nguo ni moja ya eneo ambalo wafungwa hupata huduma za urekebishwaji kwa vitendo.

Sunday, January 27, 2019

GEREZA KITETE – NKASI LAANZA UZALISHAJI WA ZAO LA MAHARAGE


Na ASP. Lucas Mboje, Nkasi

KATIKA kuelekea kwenye mpango wa kujitosheleza kwa chakula cha wafungwa magerezani Gereza la Kilimo Kitete – Nkasi limeanza uzalishaji wa maharage ambapo katika msimu huu wa mwaka 2018/2019 tayari limelima zao hilo.

Akizungumza leo mara baada ya kutembelea Gereza hilo, Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike amesema kuwa ameridhishwa na hatua mbalimbali zinazoendelea katika kufanikisha mpango mkakati wa uzalishaji wa chakula kwa wingi katika maeneo yakimkakati pamoja na uwepo wa changamoto mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya hali ya hewa na vitendea kazi.

“Ni lazima tuhakikishe kuwa jukumu hili tulilopewa linatekelezwa ipasavyo hivyo, Mkuu wa Gereza pamoja na timu yako hakikisheni mnaongeza bidii ya kazi kwa kutumia rasilimali zilizopo ikiwemo nguvu kazi ya wafungwa ili kufikia malengo ya hekari 300 za zao la maharge mlizopewa kwani msimu bado unaruhusu”. Alisema Kamishna Jenerali Kasike.

Aidha, Kamishna Jenerali Kasike amesema kuwa Jeshi litaangalia uwezekano wa kuliwezesha Gereza Kitete zana mbalimbali za kilimo kama vile trekta, ambazo zitarahisisha kufanikisha malengo ya kimkakati ili kuongeza uzalishaji wa chakula cha wafungwa.

Ameongeza kuwa Gereza Kitete - Nkasi ni miongoni mwa magereza 10 ya kimkakati ambayo tayari yameainishwa katika mpango mkakati wa Jeshi la Magereza katika kujitosheleza kwa chakula cha wafungwa. Magereza mengine ni Songwe, Mollo, Arusha, Idete, Kiberege, Kitengule, Pawaga, Kitai na Gereza Ludewa.

Katika hatua nyingine, Kamishna Jenerali Kasike amewaasa viongozi wa Jeshi hilo pamoja na watendaji waliopewa dhamana ya kusimamia vitengo(Ugavi na Uhasibu) katika vituo vyao kuzingatia suala la uadilifu na amewataka kujiepushe na vitendo vyote vya ubadhilifu wa mali za umma ili kuwezesha kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza Kitete, SP. Job Lwesya alisema kuwa  katika msimu wa Kilimo wa mwaka 2018/2019 gereza hilo limelima ekari 114 za maharage na kwa sasa linaendelea na maandalizi ya mashamba mengine ili kufikia malengo waliyopewa ya kulima hekari 300 za maharage.

Aidha, aliongeza kuwa  gereza hilo linayo ardhi ya kutosha na yenye rutuba hivyo wamejipanga kimkakati katika kuhakikisha kuwa wanazalisha mazao mbalimbali kwa wingi kwa ajili ya chakula wafungwa.

Gereza Kitete - Nkasi lina eneo lenye ukubwa wa ekari 3,742 ambazo zinafaa kwa kilimo cha mazao mbalimbali ya chakula ikiwemo zao la maharage, mahindi na Alizeti. Gereza hilo lilianzishwa rasmi mwaka 1989 kwa lengo la kuwahifadhi wahalifu pamoja na kuwapatia wafungwa programu za urekebishaji ili wamalizapo vifungo vyao waweze kuwa raia wema.



Thursday, January 24, 2019

KAMISHNA JENERALI WA MAGEREZA, PHAUSTINE KASIKE AWASILI JIJINI MBEYA LEO TAYARI KWA ZIARA YA KIKAZI KATIKA BAADHI YA MIKOA YA NYANDA ZA JUU KUSINI

Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike(kulia vazi la kiraia) akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Songwe leo Januari 24, 2019 tayarri kwa ziara ya kikazi katika baadhi ya mikoa ya nyanda za juu kusini ikiwemo Mbeya, Songwe, Rukwa, Katavi na Ruvuma.


Kutoka kulia ni Mkuu wa Gereza Kuu Ruanda Mbeya, SSP Lugona Msomba, Mkuu wa Chuo cha Mafunzo ya awali ya Uaskari Magereza – Kiwira, ACP. Mathias Mkama, Mkuu wa Chuo cha Ufundi Ruanda Mbeya, SSP. Enock Lupyuto kwa pamoja wakiteta jambo kabla ya mapokezi ya Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini leo Januari 24, 2019 jijini Mbeya.


Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike(vazi la kiraia) akisalimiana na Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Mbeya mapema  alipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Songwe leo Januari 24, 2019 kwa ziara ya kikazi katika baadhi ya mikoa ya nyanda za juu kusini.

Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine Kasike(katikati vazi la kiraia) akiteta jambo na Maafisa Waandamizi wa Jeshi hilo mara baada ya kuwasili jijini Mbeya kwa ziara ya kikazi(kulia) ni Mkuu wa Magereza Mkoani Mbeya, SACP. Luhende Makwaia(wa kwanza kushoto) ni Mkuu wa Chuo cha Mafunzo ya awali ya Uaskari Magereza – Kiwira, ACP. Mathias Mkama(wa pili toka kushoto) ni Mkuu wa Magereza Mkoani Mbeya, ACP. Lyzek Mwaseba.(Picha zote na Jeshi la Magereza).

Tuesday, January 1, 2019

SALAAM ZA KAMISHNA JENERALI WA MAGEREZA PHAUSTINE KASIKE KWA WATUMISHI WA JESHI HILO KATIKA KUFUNGA MWAKA 2018 NA KUUKARIBISHA MWAKA 2019 TAREHE 31 DEC, 2018



Na ASP Deodatus Kazinja

Katika kufunga mwaka 2018 na kuukaribisha mwaka 2019  Kamishna Jenerali wa Magereza, Phaustine Kasike ameelezea matarajio ya Jeshi hilo kwa mwaka 2019 kuwa ni pamoja  kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali zikiwemo asasi za kiraia katika kutoa huduma kwa wafungwa na mahabusu.

Matarajio mengine ni pamoja na  kuimarisha hali ya ulinzi na usalama magerezani ikiwa ni pamoja na kusimika mifumo ya kiusalama, kujenga kiwanda cha seremala mkoani Dodoma ili kuongeza na kuimarisha  utengenezaji wa samani, kujenga nyumba 100 mkoani Dodoma kwa ajili ya watumishi wa ofisi ya Makao makuu mkoani humo.

Aidha, Kamishna Jenerali Kasike ameongeza kuwa matarajio ya mwaka ujao ni  Kuanzisha ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Makao Makuu mkoani Dodoma, kuendelea kuhimiza ujenzi wa nyumba kwa njia ya kujitolea ili kupunguza uhaba wa nyumba za watumishi wa jeshi hilo,

Pia amesema atahakikisha Shirika la Magereza (Magereza Corporation Sole) linapata Bodi ili kujiimarisha katika kufanya shughuli za kibiashara.

 Ameongeza kuwa Jeshi la Magereza litashirikiana na Idara ya mahakama katika kukamilisha maandalizi ya uendeshaji wa mashauri kwa mfumo wa kielektroniki wa ‘video conference’ ili kurahisisha utoaji wa haki kwa wafungwa na mahabusu kwa wakati.
Kamishna Jenerali Kasike amehitimisha Salaam za Mwaka Mpya kwa kusisitiza suala la ufanyaji kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zinazoongoza Jeshi hilo na amewataka askari kubadili mtazamo wa kiutendaji na kuacha kufanya kazi kwa mazoea. “Kila mmoja atimize wajibu wake kikamilifu kwa kutumia uweledi, ubunifu na kutanguliza maslahi ya Taifa mbele”.
Kamishna Jenerali wa Magereza Phaustine Kasike (kushoto) akiwasili tayari katika Baraza la kufunga mwaka 2018 na kuukaribisha mwaka 2019  Desemba 31, 2018 Makao Makuu ya Jeshi la Magereza

Kamishna Jenerali wa Magereza Phaustine Kasike akizungumza na maafisa na askari wa Jeshi la Magereza katika Baraza la kufunga mwaka 2018 na kuukaribisha mwaka 2019  Desemba 31, 2018 Makao Makuu ya Jeshi la Magereza

Baadhi ya maafisa, askari na watumishi raia wa Jeshi la Magereza wakimsilikiliza  Kamishna Jenerali wa Magereza Phaustine Kasike (hayupo pichani)wakati wa Baraza la kufunga mwaka 2018 na kuukaribisha mwaka 2019  Desemba 31, 2018 Makao Makuu ya Jeshi la Magereza

Baadhi ya Maafisa wa Jeshi la Magereza wakiwa wamesimama kwa heshima kuwakumbuka watumishi mbalimbali wa jeshi hilo walioaga dunia kwa mwaka 2018. (Picha zote na Jeshi la Magereza)