Banner

Banner

Saturday, March 29, 2025

WAHITIMU WA KOZI YA UONGOZI WA JESHI LA MAGEREZA WATAKIWA KUONESHA WELEDI KAZINI


Naibu Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri wa Nishati, Mhe. Dotto Biteko (Mb), ametoa Wito kwa  Wahitimu wa Kozi ya Uongozi wa Ngazi ya Juu (GO'S) Jeshi la Magereza, kutumia maarifa waliyopata kuboresha utendaji kazi, kudumisha nidhamu, sambamba na kuleta magaeuzi chanya ndani ya jeshi.

Mhe. Biteko amezungumza hayo katika hafla ya kufunga Kozi namba 27 ya Uongozi wa juu iliyofanyika katika viwanja vya Chuo Cha Taaluma ya Sayansi ya Urekebishaji Tanzania (TCTA) jijini Dar es Salaam, Machi 28, 2025 ambapo aliwapongeza wahitimu kwa hatua waliyoifikia na kuwakumbusha kuwa kupandishwa cheo ni ishara ya kuongezewa majukumu makubwa zaidi.

"Serikali inatarajia kuona mnakuwa chachu ya mabadiliko katika Jeshi la Magereza kwa kufanya kazi kwa bidii, uadilifu, na kuhakikisha haki inatendeka kwa mujibu wa Sheria," alisema Mhe. Biteko.

Naibu Waziri Mkuu, Alisisitiza kuwa Jeshi la Magereza lina jukumu kubwa la kuwahudumia watu waliokosea, lakini lengo kuu ni kuwasaidia kurekebisha tabia zao ili wawe raia wema wanaporejea kwenye jamii. Aliwataka wahitimu kuhakikisha wanazingatia utu, weledi na kuzingatia Sheria, taratibu na kanuni za kazi.

Kwa Upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Daniel Sillo amesisitiza dhamira ya Serikali ya kuleta mageuzi katika Taasisi za Haki Jinai kama sehemu ya juhudi za kuboresha mifumo ya utoaji haki nchini.

Aliongeza kuwa hatua hiyo inatokana na maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye aliunda Tume Maalum ya Kuboresha Taasisi za Haki Jinai ili kutathmini changamoto zilizopo na kupendekeza njia bora za kuimarisha Sekta hiyo.

Naye, Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza (CGP) Jeremiah Katungu, amesema kuwa, Jeshi kwa kushirikiana na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) lilizindua mpango wa kurasimisha ujuzi wa wafungwa, ambapo jumla ya wafungwa 201 wamepatiwa vyeti rasmi. Lengo la mpango huo ni kuhakikisha ujuzi walioupata Magerezani unatambulika rasmi ili kuwawezesha kupata ajira au kujiajiri mara baada ya kumaliza vifungo vyao.

Tuesday, March 18, 2025

KAMATI YA BUNGE YA AFYA NA MASUALA YA UKIMWI YAFANYA UKAGUZI ZAHANATI YA GEREZA SINGIDA.

 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya Ukimwi, ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Hassan Mtenga, imefanya ziara ya ukaguzi katika  Zahanati ya Gereza Singida, leo machi 17, 2025, ikiwa na lengo la kutathmini huduma zinazotolewa zahanati hapo.

 

Katika ukaguzi huo  Kamati ilikagua huduma za CTC, chumba  cha Maabara, chumba cha daktari, chumba cha takwimu pamoja na chumba cha  dawa,  pia  waliweza kufanya  kikao na Kamati ya mkoa ya Afya  na masuala  ya  Lishe  na kuupongeza uongozi wa  jeshi la magereza kwa huduma  wanazotoa katika zahanati hiyo.


"Hongereni kwa kazi kubwa na nzuri ambayo  mnafanya, tumejionea ,  DMO pamoja na  dactari mkuu wa mkoa  tunaomba  mtatue changamoto ndogondogo zinazokabili  zahanati ya gereza" alisema  Mhe. Mtenga


Aidha Mhe. Mtenga ametoa rai kwa Wajumbe wa Kamati hiyo pamoja na wabunge wote nchini  kujenga utamaduni wa kutembelea  Magereza mbalimbali ili kubaini changamoto zinazoyakabili na kuzitafutia ufumbuzi.


Kwaupande wake Kamishina Jenerali wa  Magereza  Jeremia  Yoram Katungu  ameishukuru  Kamati ya Bunge  ya Afya na Masuala ya  Ukimwi kwa kutembelea na kukagua Zahanati hiyo na kuahidi kuyafanyia kazi maelekezo yote waliyoyatoa ili kuboresha huduma za Afya

Monday, March 17, 2025

KAMATI YA BUNGE MAMBO YA NJE ULINZI NA USALAMA (NUU) YATEMBELEA GEREZA KUU ISANGA.


Kamati ya Bunge Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama (NUU) ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Vita Kawawa, Machi 13,2025,  wametembelea Gereza Kuu Isanga jijini Dodoma kujionea miradi mbalimbali inayoendelea katika Gereza hilo pamoja na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Gereza Maalum.


Akizungumza mara baada ya ukaguzi ujenzi wa Gereza Maalum, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Vita Rashid Kawawa ameonesha kuridhishwa na maendeleo ya ujenzi na kulipongeza Jeshi la Magereza kwa kusimamia kikamilifu Fedha za Serikali katika kutekeleza mradi.


‎Aidha Kamati hiyo imelipongeza Jeshi la Magereza kwa kutekeleza agizo la Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia vema matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwemo matumizi ya mkaa mbadala(Briquettes),Gas asili(Natural Gas) magerezani na kufanikisha kuondokana na nishati chafu. 

‎Kwa upande wake Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza (CGP) Jeremiah Katungu ameishukuru kamati hiyo kwa mafanikio aliyoyapata kwa bajeti ya mwaka 2023/24 na kufanikisha ukarabati wa Gereza maalum liliopo eneo la Gereza kuu Isanga.

‎"Jeshi linaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama kwa namna anavyoliwezesha Jeshi la Magereza katika kutekeleza majukumu yake ya msingi ikiwemo miradi ya kimaendeleo" alisema CGP. Jeremiah Katungu.

ZIARA YA NDC MAKAO MAKUU YA MAGEREZA


Wakufunzi na wanafunzi kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC),leo Machi 12,2025 wamefanya ziara Makao Makuu ya Jeshi la Magereza Msalato jijini Dodoma, lengo likiwa ni kujifunza shughuli mbalimbali zinazofanywa na Jeshi la Magereza.

Akiongea katika hotuba yake Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza (CGP)Jeremiah Yoram Katungu amekipongeza Chuo hicho kwa kufanya ziara Makao Makuu ya Jeshi la Magereza huku akisema uhusiano huo unalenga kujenga na kuimarisha katika muktadha wa kulinda mataifa yetu kuendelea.

Kwa upande wake Brigedia Jenerali C.J.Ndiege ambaye ni mkuu wa msafara kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) amesema kuwa miongoni mwa malengo ya Chuo hicho ni kutoa mafunzo ya kimkakati katika masuala ya ulinzi kwa sekta binafsi, kikanda na kimataifa.

Aidha katika ziara hiyo kulitolewa wasilisho la matumizi ya teknologia ya habari magerezani,ambapo wasilisho hilo lilitolewa na Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Kizito Jaka.


Pamoja na mambo mengine washikiri katika ziara hiyo walipata fursa ya kupanda miti eneo linalozunguka Makao Makuu ya Jeshi la Magereza.

WAZIRI BASHUNGWA ATUNUKU VYETI KWA WAFUNGWA 201 WALIOHITIMU MAFUNZO GEREZANI

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Innocent Lugha Bashungwa (Mb), leo Machi 11, 2025 amezindua Programu ya Urasimishaji wa ujuzi uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa mafunzo (Recognition of Prior Learning - RPL) na kuwatunuku vyeti vinavyo tambulika na VETA Wafungwa 201 waliohitimu Mafunzo ya fani mbalimbali yaliyotolewa na Jeshi la Magereza.


Akizungumza katika hafla hiyo ya utoaji vyeti Mhe. Bashungwa alisema Programu hiyo itatoa hamasa kwa wafungwa kujifunza na kushiriki kikamilifu katika shughuli mbalimbali za urekebishaji ili kupata ujuzi, elimu, na maarifa kwa ajili ya kuwasaidia kujiajiri au kuajiriwa pindi watakaporudi katika jamii baada ya kutumikia vifungo vyao magerezani. 


Kwaupande wake Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza (CGP) Jeremiah Yoram Katungu, ameishukuru Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi stadi (VETA) kwa kukubali kuingia makubaliano na Jeshi la Magereza na kutoa vyeti kwa Wafungwa wanohitimu fani mbalimbali Magerezani.


Hafla ya utoaji vyeti kwa Wafungwa ilifanyika Chuo KPF Mkoani Morogoro ambapo Wafungwa waliotunukiwa vyeti wamehitimu katika fani ya Umeme, Ujenzi, ufundi rangi, bomba, magari, upishi, ushonaji na Seremala.