MADEREVA wote wa magari ya Jeshi la Magereza nchini wametakiwa kuzingatia Sheria za Usalama Barabarani wakati wote wanapoendesha magari ili kujiepusha na ajali zisizo za lazima.
Rai hiyo imetolewa na Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, John Casmir Minja wakati akizungumza kwenye hafla ya kufunga Mafunzo ya Udereva Kozi ya Msasa kwa Maofisa wa Jeshi la Magereza kutoka Mikoa yote Tanzania Bara yaliyofanyika katika Chuo cha Udereva na Ufundi, Kingolwira Mkoani Morogoro.
Jenerali Minja amewaagiza Wahitimu wa Mafunzo hayo kuhakikisha kuwa wanawajibika pia kuyatunza magari watakayokabidhiwa kuyaendesha ili yaweze kudumu kwa muda mrefu kama ilivyokusudiwa.
"Nawataka mjiepushe na uzembe wakati mnapoendesha magari ya Jeshi letu ikiwa ni pamoja na kutokujihusisha na ulevi na kuendesha magari hayo kwa mwendo kasi bila kuzingatia Sheria za Usalama Barabarani". Alisema Jenerali Minja.
Aidha Jenerali Minja amezungumzia upungufu mkubwa wa magari katika Jeshi hilo ambapo katika kushughulikia changamoto hiyo Jeshi la Magereza kupitia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa limesaini Mkataba na Kampuni za Ashok Layland na Jeep na magari mia tisa na tano(905) yanategemewa kupokelewa mapema mwanzoni mwa mwezi Mei Mwaka huu.
Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Udereva na Ufundi Kingolwira, Kamishna Msaidizi wa Magereza, Osmond Ndunguru kupitia risala yake kwa Mgeni rasmi amesema kuwa Wahitimu hao wamejifunza Mafunzo yote yaliyopo kwenye Mtaala wa Mafunzo ya Udereva kwa nadharia na vitendo ikiwemo mbinu mbalimbali katika fani ya Udereva wa Magari ambapo jumla ya Wanafunzi 125 wamehitimu Mafunzo hayo miongoni mwao Wanaume ni 133 na wa kike ni 2.
Aidha Kamishna Msaidizi wa Magereza, Nduguru alieleza changamoto mbalimbali ambazo Chuo hicho kinakabiliana nazo ikiwemo upungufu wa magari ya kujifunzia pamoja na uchakavu wa miundombinu ya majengo hali inayoathili utoaji taaluma ya mafunzo hayo.
Chuo cha Udereva na Ufundi cha Kingolwira, kilichopo Mkoani Morogoro kinamilikiwa na Jeshi la Magereza ambacho hutoa Mafunzo ya Udereva kwa Maofisa wa Jeshi la Magereza ambao huendesha magari ya Jeshi hilo na katika Taasisi mbalimbali za Umma hapa nchini.