Mojawapo ya Jukumu la Jeshi la Magereza ni kuwapeleka mahakamani mahabusu na kuwarudisha magerezani.

Gadi ya askari Wanawake na Wanaume wa Jeshi la Magereza katika Maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa.

Ng'ombe bora wa Nyama na Maziwa ni sehemu ya miradi ya Uzalishaji inayoendeshwa na kusimamiwa na Jeshi la Magereza nchini.

Sehemu ya Mashamba makubwa yanayoendeshwa na Jeshi la Magereza: Shughuli za Kilimo cha Mashamba makubwa, madogo na bustani za mboga mboga ni moja ya shughuli za Magereza katika kuwafunza wafungwa namna ya kujitegemea mara wamalizapo vifungo vyao.

Baadhi wa wafungwa katika Kiwanda cha Ushonaji nguo cha Gereza Kuu Ukonga wakiwa kazini: Shughuli za Ushonaji wa nguo ni moja ya eneo ambalo wafungwa hupata huduma za urekebishwaji kwa vitendo.

Friday, October 23, 2015

Serikali yasaini mkataba wa ununuzi wa magari na kampuni ya Ashok Leyland kwa vyombo vya ulinzi na usalama, jijini Dar

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Job Masima (kulia), Makamu wa Rais wa Kampuni ya Kutengeneza Magari ya ASHOK LEYLAND ya nchini India, Bhimasena Rau wakisaini Mkataba wa ununuzi wa magari kwa ajili ya matumizi ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama ambavyo ni Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI. Hafla hiyo ilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, jijini Dar es Salaam.  

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Job Masima (kulia), Makamu wa Rais wa Kampuni ya Kutengeneza Magari ya ASHOK LEYLAND ya nchini India, Bhimasena Rau wakipongezana baada ya kusaini Mkataba wa ununuzi wa magari kwa ajili ya matumizi ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama ambavyo ni Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI. 
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Job Masima (watatu kushoto), akitoa neno la shukrani baada ya kusaini mkataba wa ununuzi wa magari ya Kampuni ya ASHOK LEYLAND ya nchini India. Magari hayo ni kwa ajili ya matumizi ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI. Kushoto ni Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Jumanne Sagini, wapili kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mbarak Abdulwakil. 
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mbarak Abdulwakil (wapili kulia) akipokea Mkataba wa Ujenzi wa Nyumba za Makazi ya Watumishi wa Jeshi la Magereza kutoka kwa Makamu wa Rais wa Kampuni ya Ujenzi ya Poly Technologies ya nchini China. Kulia ni Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, John Casmir Minja. Halfa hiyo ilifanyika katika Ukumbi mdogo wa Mikutano wa Wizara hiyo, jijini Dar es Salaam. 
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Job Masima (katikati aliyevaa tai), Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mbarak Abdulwakil (wakumi kulia), Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI, Jumanne Sagini (wanane kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama pamoja na Viongozi wa Kampuni ya Kutengeneza Magari ya ASHOK LEYLAND ya nchini India. 


Serikali ya Tanzania imeingia Mkataba wa ununuzi wa magari kwa Vyombo vya Ulinzi na Usalama nchini na Kampuni ya Motorrama (T) LTD ambayo ni Wakala wa Magari aina ya ASHOK LEYLAND kutoka nchini India. 

Mkataba huo umesaniwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Job Masima pamoja na Makamu wa Rais wa Kampuni hiyo ya Utengenezaji wa magari, Bhimasena Rau ukishuhudiwa na Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama katika Ukumbi wa Mikutano wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza mara baada mkataba huo kusainiwa, Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, John Casmir Minja aliishukuru Serikali kwa msaada huo ambao utasaidia kutatua tatizo la uhaba wa magari katika Jeshi la Magereza. 

“Utekelezaji wa mpango huu katika Jeshi la Magereza utakuwa na manufaa makubwa kwani utapunguza tatizo la uhaba wa magari kwa ajili ya shughuli za uendeshaji na utawala pamoja na utekelezaji wa jukumu la kuwasafirisha Mahabusu kwenda mahakamani na kurudi magerezani,” alisema Minja.

 Lengo kubwa la ununuzi wa Magari hayo unalenga kuboresha huduma za usafiri pamoja na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama hapa nchini. 


Picha zote na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi


Saturday, October 17, 2015

Mahafali ya kidato cha nne shule ya sekondari Bwawani inayomilikiwa na Jeshi la Magereza yafana mkoani Pwani

Mgeni rasmi Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Bw. Mbarak Abdulwakil akimkabidhi cheti Mwanafunzi Mhitimu kwenye Mahafali ya Kumi na mbili ya Kidato cha Nne katika Shule ya Sekondari Bwawani Oktoba 16, 2015(kulia kwa Mgeni rasmi) ni Kamishna Jenerali wa Magereza, John Casmir Minja.
Baadhi ya Wahitimu Kidato cha Nne Shule ya Sekondari Bwawani inayomilikiwa na Jeshi la Magereza wakipiga makofi wakati wa hotuba ya Mgeni rasmi Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mbarak Abdulwakil(hayupo pichani).
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Bw. Mbarak Abdulwakil(katikati) akiwa na Viongozi mbalimbali Meza Kuu wakiimba wimbo wa Shule ya Sekondari Bwawani kwenye hafla ya Mahafali ya Kidato cha Nne ya shule hiyo(wa pili kushoto) ni Kamishna Jenerali wa Magereza, John Casmir Minja(wa pili kulia) ni Mwenyekiti wa Bodi ya Shule, Kamishna wa Magereza wa Utawala na Fedha, Gaston Sanga
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Bw. Mbarak Abdulwakil(kulia) akisoma jiwe la msingi la Jengo la Maabara ya masomo ya Sayansi kama anavyoonekana katika picha.
Muonekano wa nje wa Jengo la Maabara ya Masomo ya Sayansi katika Shule ya Sekondari ya Bwawani baada ya Mgeni rasmi kuweka jiwe la msingi.
Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini, John Casmir Minja akitoa maelezo mafupi kabla ya kumkaribisha Mgeni rasmi kwenye Mahafali ya Kidato cha Nne Shule ya Sekondari Bwawani.
Baadhi ya Walimu na Wafanyakazi wa Shule ya Sekondari Bwawani wakifuatilia kwa makini maelezo ya Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza kwenye Mahafali hayo ya Kidato cha Nne.
Wahitimu wa kidato cha nne katika shule ya Sekondari Bwawani wakigani shairi lao mbele ya Mgeni rasmi.



Na Lucas Mboje, Pwani

Wahitimu wa kidato cha nne nchini wameaswa kuachana na fikria potofu kuwa elimu wanayoipata itawapatia ajira Serikalini au kwenye Sekta binafsi badala yake watumie elimu hiyo kama nyenzo muhimu ya kuwawezesha kujiajiri wao wenyewe.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya ndani ya nchi, Bw. Mbarak Abdulwakil alipokuwa mgeni rasmi wakati wa mahafali ya kumi na mbili ya kidato cha nne katika shule ya Bwawani Sekondari iliyopo Mkoani Pwani.

"Katika hali ya sasa ya utandawazi yapo mambo kadhaa ambayo mtu binafsi anaweza kuyafanya na kujipatia kipato cha kujiendeleza maisha yake". Alisema Bw. Abdulwakil.

Bw. Abdulwakil amesisitiza kuwa wanachotakiwa kufanya wahitimu hao ni kuyasoma mazingira ya maisha popote watakapokuwa na kuamua namna ya kujiajiri ili mradi isiwe shughuli zinazopingana na sheria na maadili ya kijamii, kama vile kuuza madawa ya kulevya, ukahaba, unyang'anyi na mambo mengine yanayofanana na hayo.

Awali akimkaribisha Mgeni rasmi Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini, John Casmir Minja alisema kuwa uongozi wa Jeshi la Magereza kwa kushirikiana na Bodi ya shule utaendelea kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbalimbali zinazozikabili shule hiyo kadri uwezo wa kifedha unavyopatikana.

Jeneral Minja alizitaja baadhi ya changamoto mbalimbali ambazo tayari zimefanyiwa kazi ikiwemo miradi ya miundo mbinu ya msingi kama vile Madarasa, Maabara, Maktaba na mradi wa maji ambapo kwa kiasi kikubwa miradi hiyo imechangia kuboresha maendeleo ya kitaaluma shuleni hapo.

Kwa upande wake Mkuu wa shule ya Sekondari Bwawani, Kamishna Msaidizi wa Magereza, Emmanuel Lwinga alipokuwa akitoa taarifa fupi kwa mgeni rasmi katika mahafali hayo amesema kuwa shule yake ni miongoni mwa shule nchini ambazo zinafanya vizuri kitaaluma na masuala mengineyo yasiyoyakitaaluma.

Aliongeza kuwa mwaka 2014 kati ya wanafunzi 95 waliofanya mitihani ya kidato cha nne katika shule hiyo wanafunzi 87 sawa na asilimia 91.6% walifaulu, aidha wanafunzi 52 walichaguliwa kujiunga na masomo ya Kidato cha Tano katika shule mbalimbali za serikali.

Shule ya Sekondari Bwawani inamilikiwa na Jeshi la Magereza, ilianzishwa Mwaka 1978 kwa lengo la kutoa elimu ya Sekondari kwa Watumishi wa Magereza ambapo hivi sasa shule hiyo inatoa elimu kwa vijana wa kike na kiume kutoka maeneo mbalimbali hapa nchini kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita.

Thursday, October 15, 2015

Taarifa kwa vyombo vyahabari

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Bw. Mbarak Abdulwakil kesho Oktoba 16, 2015 anatarajia kuwa Mgeni rasmi kwenye sherehe za Mahafali ya kumi na mbili ya Kidato cha Nne katika Shule ya Sekondari ya Bwawani iliyopo Mkoa wa Pwani.


Bofya hapa kupata taarika kamili

Katibu mkuu wizara ya mambo ya ndani ya nchi mgeni rasmi katika mahafali ya kidato cha nne shule ya sekondari Bwawani

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Bw. Mbarak Abdulwakil

Na Lucas Mboje, Dar es Salaam;

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Bw. Mbarak Abdulwakil(pichani) kesho Oktoba 16, 2015 anatarajia kuwa Mgeni rasmi kwenye sherehe za Mahafali ya kumi na mbili ya Kidato cha Nne katika Shule ya Sekondari ya Bwawani iliyopo Mkoa wa Pwani.

Kwa mujibu wa Taarifa kwa Vyombo vya Habari iliyotolewa leo Jijini Dar es Salaam na kusainiwa na Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, John Casmir Minja inasema jumla ya Wanafunzi 95 wa Shule hiyo wanatarajia kuhitimu elimu yao ya Kidato cha Nne Novemba Mwaka huu.

Taarifa hiyo inasema Mgeni rasmi atafanya mambo yafuatayo ikiwemo kuweka jiwe la msingi jengo la maabara, uzinduzi wa mradi wa maji kwenda kwenye majengo ya Kidato cha tano na sita, kuangalia Maonesho ya Taaluma kwa Wanafunzi Washiriki, kutoa vyeti na zawadi mbalimbali kwa Wanafunzi wahitimu na kutoa hotuba.

Shule ya Sekondari Bwawani inamilikiwa na Jeshi la Magereza, ilianzishwa Mwaka 1978 kwa lengo la kutoa elimu ya Sekondari kwa Watumishi wa Magereza ambapo hivi sasa Shule hiyo inatoa elimu ya Sekondari kwa Vijana wa kike na kiume kutoka maeneo mbalimbali hapa nchini kuanzia Kidato cha kwanza hadi cha sita.