Hafla ya makabidhiano hayo yamefanyika leo tarehe 28 Julai, 2016 katika Viwanja vya Shule ya Msingi Chamazi iliyopo Wilaya ya Temeke, Jijini Dar es salaam ambapo Waziri Mkuu Majaliwa amekabidhi madawati katika Shule ya Msingi Chamazi yaliyotolewa na Ubalozi wa Kuwait nchini Tanzania na Jumuiya ya Mabohora Tanzania kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Mkuu Majaliwa amewashukuru na kuwapongeza Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kutoa mchango huo na pia amewapongeza wadau wengine ambao wameitikia wito wa Rais Magufuli wa kuchangia madawati kwa lengo la kuondoa tatizo la wanafunzi kukaa chini.
Waziri Mkuu Majaliwa amesema baada ya kuanza kutekeleza ahadi ya kuondoa ada kwa shule za msingi na sekondari, idadi ya wanafunzi waliojiandikisha kuanza darasa la kwanza katika shule mbali mbali imeongezeka hali iliyosababisha upungufu wa madawati lakini tatizo hilo limetatuliwa kwa kiasi kikubwa hapa nchini.
Aidha, amelitaka na Jeshi la Magereza kutengeneza madawati hayo mapema iwezekanavyo ili yakamilike haraka na kuanza kutumika katika Shule za Msingi Majimatitu na Mbande kwani shule hizo zinakabiliwa na idadi kubwa ya Wanafunzi hapa Jijini Dar es Salaam.
Hafla hiyo imehudhuriwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Ramadhani Mwinyi, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Paul Makonda, Wakuu wa Wilaya zote za Mkoa wa Dar es Salaam, Wakurugenzi wote wa Halmashauri za Mkoa wa Dar es Salaam, Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Dar es Salaam, Wananchi pamoja na wanafunzi wa Shule ya msingi Chamazi.
Lucas Mboje, Mrakibu Msaidizi wa Magereza,
Afisa Habari wa Jeshi la Magereza,
Makao Makuu ya Jeshi la Magereza,
28 Julai, 2016.