Friday, September 18, 2015

Katibu mkuu wizara ya mambo ya ndani ya nchi azindua huduma za "Duty Free Shop" magereza mkoani Arusha

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mbarak Abdulwakil(wa pili kushoto)akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa Huduma za Magereza Duty free shop Mkoani Arusha leo Septemba 18, 2015 katika Viwanja vya Gereza Kuu Arusha(wa kwanza kulia) ni Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, John Casmir Minja(wa pili kulia) ni Mkurugenzi Mtendaji wa Dar Smart LTD, Bw. Mohamed Panjwani.
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mbarak Abdulwakil(kulia)akisoma jiwe la Msingi kwenye hafla ya uzinduzi wa Duty free shop ya Magereza Mkoani Arusha(kushoto) ni Kamishna Jenerali wa Magereza, John Casmir Minja.
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza Nchini, John Casmir Minja akitoa maelezo mafupi wakati wa kumkaribisha Mgeni rasmi katika hafla ya uzinduzi wa Huduma za Duty free shop ya Magereza Mkoani Arusha.
Askari wa Jeshi la Magereza kutoka Magereza mbalimbali yaliyopo Mkoani Arusha wakifuatilia kwa makini hotuba ya Mgeni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mbaraka Abdulwakil(hayupo pichani).
 Bidhaa za majumbani zinazopatikana katika Duty free shop ya Magereza Mkoani Arusha
Mgeni rasmi Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mbarak Abdulwakil(katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoani Arusha waliosimama mara tu baada ya kuzindua Huduma za Duty free shop ya Magereza Mkoani Arusha(wa pili kushoto) ni Kamishna Jenerali wa Magereza, John Casmir Minja(wa pili kulia) ni Mkuu wa Magereza Mkoani Arusha, SACP. Hamis Nkubasi(wa kwanza kushoto) ni Mkuu wa Magereza Mkoani Kilimanjaro, SACP. Venant Kayombo(wa kwanza kulia) ni Mkurugenzi Mtendaji wa Dar Mart LTD, Bw. Mohamed Panjwani


Na Lucas Mboje, Arusha
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mbarak Abdulwakil amepongeza kasi ya Utendaji kazi wa Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, John Casmir Minja pamoja na Uongozi wote wa Jeshi hilo kwa kutekeleza kwa mafanikio makubwa mpango wa Serikali ya Awamu ya Nne wa kuwasogezea huduma za bidhaa muhimu na zenye manufaa Maafisa, askari Magereza na familia zao katika maeneo yao ya kazi hususani huduma za "Duty free shops".
Mhe. Mbarak Abdulwakil ameyasema hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa "Duty free shop"ya Magereza Mkoani Arusha iliyofanyika leo Septemba 18, 2015 katika Viwanja vya Gereza Kuu Arusha ambapo baadhi ya Viongozi mbalimbali wa Kiserikali na Binafsi wa Mkoa wa Arusha walihudhuria hafla hiyo.
"Nampongeza kwa dhati Kamishna Jenerali wa Magereza John Casmir Minja kwa jitihada hizi ambapo matunda yake yanaonekana na amethibitisha kwamba azma ya kusambaza huduma hii nchi nzima ipo pale pale na jitihada zinaonekana". Alisema Abdulwakil.

Ameongeza kuwa lengo la Mpango huu ni kuhakikisha kuwa ustawi wa maisha ya Maafisa na Askari wa Majeshi yote ya Ulinzi na Usalama unatekelezwa ipasavyo kwa kuwapatia bidhaa zenye bei nafuu ili kuwapunguzia ukali wa maisha.

Aidha, Mhe. Abdulwakil amewaasa Maafisa na askari watakaotumia huduma husika kuzingatia Sheria, Kanuni na taratibu pamoja na maadili ya uendeshaji wa maduka hayo ili kuhakikisha kuwa adhima ya Serikali ya kuwapunguzia makali ya maisha Maafisa, askari pamoja na familia zao wananufaika ipasavyo na si vinginevyo.

Awali akimkaribisha Mgeni rasmi,Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, John Casmir Minja alisema kuwa Jeshi la Magereza kwa kushirikiana na Kampuni ya Dar Mart LTD limeazimia kusambaza huduma za Duty Free Shop nchi nzima kwa ajili ya kutoa huduma kwa Maafisa na askari.

Kamishna Jenerali Minja alimhakikishia Mgeni rasmi kuwa maduka hayo yataendeshwa kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na taratibu za "Duty Free Shop" na akasema kuwa hata sita kuchukua hatua kali za kinidhamu kwa Maafisa na askari watakao kwenda kinyume na uendeshaji wa huduma hizo.

Hivi sasa Jeshi la Magereza limefanikiwa kuzindua jumla ya "Duty Free Shops" tisa(09) ikiwemo Gereza Kuu Ukonga na Keko - Dar es Salaam, Gereza Isanga - Dodoma, Gereza Kuu Karanga - Moshi, Gereza Butimba - Mwanza, Gereza Ruanda - Mbeya, Gereza Lilungu - Mtwara, Gereza Uyui - Tabora, Chuo KPF - Morogoro na duka la tisa(09) ni Gereza Kuu Arusha.


(Picha zote na Lucas Mboje wa Jeshi la Magereza).