Na
Lucas Mboje - Jeshi la Magereza;
Jeshi la Magereza limetiliana saini
makubaliano na Asasi ya kiraia katika kuendesha
mafunzo ya ujasiriamali kwa wafungwa vijana wenye umri wa kati ya miaka
18 hadi 30 waliopo magerezani katika Mikoa ya nyanda za juu Kusini ikiwemo
Mbeya, Songwe, Iringa, Njombe, Ruvuma, Katavi na Rukwa.
Hafla ya kutiliana saini makubaliano
hayo imefanyika katika Ofisi za Makao Makuu ya Jeshi la Magereza jijini Dar es
Salaam na Asasi ya TECHNOSERVE iliwakilishwa na Afisa wake Bw. Monsiapile
Kajimbwa.
Akizungumza baada ya kutiliana saini
makubaliano hayo, Kamishna Jenerali wa Magereza, Dkt. Juma Malewa amesema kuwa
mafunzo hayo ya ujasiriamali yatawapa uwezo wafungwa wa kubaini na kutumia
fursa mbalimbali za kiuchumi ikiwemo uwezo wa kubuni na kuandaa mipango ya
biashara.
“Mafunzo haya yatawanufaisha sana
wafungwa waliopo magerezani katika mikoa hiyo kwani yatawajengea uwezo wa
kujitambua pamoja na kujipatia vipato halali badala ya kutenda uhalifu katika
jamii.” Alisema Jenerali Malewa.
Ameongeza kuwa mafunzo hayo yatafanyika
katika Chuo cha Ufundi cha Magereza Ruanda kilichopo Mkoa wa Mbeya ambapo
wafungwa watajifunza nadharia na vitendo katika dhana nzima ya ujasiriamali ikiwemo
stadi za utengenezaji sabuni, ushonaji, useremala, ufumaji sambamba na uandaaji
wa mipango ya kibiashara.
Meneja Mkazi wa Asasi ya TECHNOSERVE,
Bw. Monsiapile Kajimbwa amesema kuwa hatua ya kutiliana saini makubalino hayo
ni kuimarisha ushirikiano kati ya Asasi yake na Jeshi la Magereza katika kutoa
mafunzo kwa wafungwa ili waweze kupata ujuzi kupitia program hiyo.
Dira ya Jeshi la Magereza ni kuwa Jeshi
la kurekebisha wahalifu lenye utaalam wa hali ya juu linaloendeshwa katika
kanuni na viwango vilivyowekwa Kitaifa na Kimataifa.
Kamishna
Jenerali wa Jeshi la Magereza, Dkt. Juma
Malewa(meza kuu mbele) akisaini Mkataba wa makubaliano baina ya Asasi ya TECHNOSERVE katika mradi wa mafunzo ya
ujasiriamali kwa Wafungwa waliopo magerezani. Kulia ni Meneja Mkazi wa Asasi ya
hiyo Bw. Monsiapile Kajimbwa akisaini mkataba huo. Hafla fupi ya utilianaji saini Mkataba
huo Machi 19, 2018 Makao Makuu ya Jeshi la Magereza, Jijini Dar
es Salaam.
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, Dkt. Juma
Malewa(kushoto) na Meneja Mkazi wa Asasi ya TECHNOSERVE, Bw. Monsiapile Kajimbwa(kulia) wakionesha nyaraka za Mkataba wa makubaliano mara baada ya utiliananji wa mkataba
huo wa mradi wa mafunzo ya ujasiriamali
kwa Wafungwa waliopo magerezani.
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, Dkt. Juma
Malewa akipongezana na Meneja Mkazi wa Asasi ya TECHNOSERVE, Bw. Monsiapile Kajimbwa mara baada ya kubadilishana Mkataba
wa makubaliano baina ya Asasi
hiyo katika mradi wa mafunzo ya ujasiriamali kwa Wafungwa waliopo magerezani.
Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Magereza wakishuhudia
utiliananji saini wa mkataba huo. Kulia ni Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa
Magereza, George Mwambashi kutoka Divisheni ya Sheria ya Magereza(kushoto) ni
Mrakibu Mwandamizi wa Magereza, Uswege Mwakahesya ambaye ni Mratibu wa Programu
za Ujasiriamali katika Jeshi la Magereza
(Picha zote na Lucas Mboje wa Jeshi la Magereza).