Friday, March 23, 2018

JESHI LA MAGEREZA KUENDESHA MAFUNZO YA UJASIRIAMALI KWA WAFUNGWA

Na Lucas Mboje - Jeshi la Magereza;
Jeshi la Magereza limetiliana saini makubaliano na Asasi ya kiraia katika kuendesha  mafunzo ya ujasiriamali kwa wafungwa vijana wenye umri wa kati ya miaka 18 hadi 30 waliopo magerezani katika Mikoa ya nyanda za juu Kusini ikiwemo Mbeya, Songwe, Iringa, Njombe, Ruvuma, Katavi na Rukwa.

Hafla ya kutiliana saini makubaliano hayo imefanyika katika Ofisi za Makao Makuu ya Jeshi la Magereza jijini Dar es Salaam na Asasi ya TECHNOSERVE iliwakilishwa na Afisa wake Bw. Monsiapile Kajimbwa.

Akizungumza baada ya kutiliana saini makubaliano hayo, Kamishna Jenerali wa Magereza, Dkt. Juma Malewa amesema kuwa mafunzo hayo ya ujasiriamali yatawapa uwezo wafungwa wa kubaini na kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi ikiwemo uwezo wa kubuni na kuandaa mipango ya biashara.

“Mafunzo haya yatawanufaisha sana wafungwa waliopo magerezani katika mikoa hiyo kwani yatawajengea uwezo wa kujitambua pamoja na kujipatia vipato halali badala ya kutenda uhalifu katika jamii.” Alisema Jenerali Malewa.

Ameongeza kuwa mafunzo hayo yatafanyika katika Chuo cha Ufundi cha Magereza Ruanda kilichopo Mkoa wa Mbeya ambapo wafungwa watajifunza nadharia na vitendo katika dhana nzima ya ujasiriamali ikiwemo stadi za utengenezaji sabuni, ushonaji, useremala, ufumaji sambamba na uandaaji wa mipango ya kibiashara.

Meneja Mkazi wa Asasi ya TECHNOSERVE, Bw. Monsiapile Kajimbwa amesema kuwa hatua ya kutiliana saini makubalino hayo ni kuimarisha ushirikiano kati ya Asasi yake na Jeshi la Magereza katika kutoa mafunzo kwa wafungwa ili waweze kupata ujuzi kupitia program hiyo.

Dira ya Jeshi la Magereza ni kuwa Jeshi la kurekebisha wahalifu lenye utaalam wa hali ya juu linaloendeshwa katika kanuni na viwango vilivyowekwa Kitaifa na Kimataifa.


Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza,  Dkt. Juma Malewa(meza kuu mbele) akisaini Mkataba  wa makubaliano baina ya Asasi ya TECHNOSERVE katika mradi wa mafunzo ya ujasiriamali kwa Wafungwa waliopo magerezani. Kulia ni Meneja Mkazi wa Asasi ya hiyo Bw. Monsiapile Kajimbwa akisaini mkataba huo.  Hafla fupi ya  utilianaji saini Mkataba huo Machi 19, 2018 Makao Makuu ya Jeshi la Magereza, Jijini Dar es Salaam.

Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, Dkt. Juma Malewa(kushoto) na Meneja Mkazi wa Asasi ya TECHNOSERVE, Bw. Monsiapile Kajimbwa(kulia) wakionesha nyaraka za Mkataba wa makubaliano mara baada ya utiliananji wa mkataba huo wa  mradi wa mafunzo ya ujasiriamali kwa Wafungwa waliopo magerezani.

Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, Dkt. Juma Malewa akipongezana na Meneja Mkazi wa Asasi ya TECHNOSERVE, Bw. Monsiapile Kajimbwa mara baada ya kubadilishana Mkataba wa makubaliano baina ya Asasi hiyo katika mradi wa mafunzo ya ujasiriamali kwa Wafungwa waliopo magerezani.

Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Magereza wakishuhudia utiliananji saini wa mkataba huo. Kulia ni Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza, George Mwambashi kutoka Divisheni ya Sheria ya Magereza(kushoto) ni Mrakibu Mwandamizi wa Magereza, Uswege Mwakahesya ambaye ni Mratibu wa Programu za Ujasiriamali katika Jeshi la Magereza  
(Picha zote na Lucas Mboje wa Jeshi la Magereza).