Banner

Banner

Wednesday, April 16, 2025

WAKUU WA MAGEREZA MIKOA NA MAGEREZA YOTE NCHINI WAPONGEZWA UTEKELEZAJI MATUMIZI YA NISHATI SAFI


Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Jeremiah Yoram Katungu amewapongeza wakuu wa Magereza mikoa na Magereza yote nchini kwa utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia.


Pongezi hizo amezitoa Aprili 15, 2025 kwenye kikao kazi kilichofanyika katika Ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Jeshi la Magereza Msalato jijini Dodoma.


"Ninayo furaha Magereza yote nchini tumeachana na matunizi ya kuni na sasa tunatumia nishati safi ya kupikia" Alisema CGP Katungu.


Pia, CGP. Katungu amewataka kutorudi nyuma katika matumizi ya kuni, badala yake waendelee kutumia nishati safi ya kupikia kama Serikali ilivyoagiza.


Aidha, CGP. Katungu, amewaeleza Wakuu wa Magereza mikoa na Magereza kuwa Jeshi la Magereza limefanya ushirikiano na taasisi ya Elimu na Mafunzo ya ufundi stadi (VETA) na hivi karibuni imeweza kutunuku vyeti wafungwa 201.


Vilevile, Jeshi la Magereza linaendelea na mazungumzo na Chuo cha Uhasibu Arusha ili kuanza kutoa masomo kwa njia ya mtandao(online) kwa kuanzia na masomo ya ujasiliamali kwa wafungwa magerezani.


Pia, CGP Katungu amewataka watumishi wote wa Jeshi la Magereza kudumisha upendo, mshikamano miongoni mwao kwaajili ya maendeleo ya Taifa.


Kwa upande wake,Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza, (CP)Nicodemus Tenga 

amewataka wakuu hao wa Magereza mikoa na Magereza yote nchini kukusanya taarifa za wafungwa wenye sifa zitakazowezesha kujadiliwa katika Bodi za Parole kwa kuwa mchakato wa kumjadili mfungwa huanzia katika Kamati za urekebishaji ya Gereza, ili wafungwa wenye sifa ya kunufaika na mpango huo wanatakiwa wapatiwe.


Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Wakuu wa Magereza mikoa na Magereza yote nchini, Mkuu wa Magereza Mkoa wa Mwanza Kamishna Msaidizi Mwandamizi (SACP) Masud Kimolo, alimshukuru Mkuu wa Jeshi la Magereza (CGP) Jeremiah Katungu nakuahidi maelekezo yote ambayo ameyatoa watayatekeleza na kufanya kazi kwa weledi wa hali ya juu kwa manufaa ya Jeshi na Taifa kwa ujumla.

Saturday, March 29, 2025

WAHITIMU WA KOZI YA UONGOZI WA JESHI LA MAGEREZA WATAKIWA KUONESHA WELEDI KAZINI


Naibu Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri wa Nishati, Mhe. Dotto Biteko (Mb), ametoa Wito kwa  Wahitimu wa Kozi ya Uongozi wa Ngazi ya Juu (GO'S) Jeshi la Magereza, kutumia maarifa waliyopata kuboresha utendaji kazi, kudumisha nidhamu, sambamba na kuleta magaeuzi chanya ndani ya jeshi.

Mhe. Biteko amezungumza hayo katika hafla ya kufunga Kozi namba 27 ya Uongozi wa juu iliyofanyika katika viwanja vya Chuo Cha Taaluma ya Sayansi ya Urekebishaji Tanzania (TCTA) jijini Dar es Salaam, Machi 28, 2025 ambapo aliwapongeza wahitimu kwa hatua waliyoifikia na kuwakumbusha kuwa kupandishwa cheo ni ishara ya kuongezewa majukumu makubwa zaidi.

"Serikali inatarajia kuona mnakuwa chachu ya mabadiliko katika Jeshi la Magereza kwa kufanya kazi kwa bidii, uadilifu, na kuhakikisha haki inatendeka kwa mujibu wa Sheria," alisema Mhe. Biteko.

Naibu Waziri Mkuu, Alisisitiza kuwa Jeshi la Magereza lina jukumu kubwa la kuwahudumia watu waliokosea, lakini lengo kuu ni kuwasaidia kurekebisha tabia zao ili wawe raia wema wanaporejea kwenye jamii. Aliwataka wahitimu kuhakikisha wanazingatia utu, weledi na kuzingatia Sheria, taratibu na kanuni za kazi.

Kwa Upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Daniel Sillo amesisitiza dhamira ya Serikali ya kuleta mageuzi katika Taasisi za Haki Jinai kama sehemu ya juhudi za kuboresha mifumo ya utoaji haki nchini.

Aliongeza kuwa hatua hiyo inatokana na maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye aliunda Tume Maalum ya Kuboresha Taasisi za Haki Jinai ili kutathmini changamoto zilizopo na kupendekeza njia bora za kuimarisha Sekta hiyo.

Naye, Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza (CGP) Jeremiah Katungu, amesema kuwa, Jeshi kwa kushirikiana na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) lilizindua mpango wa kurasimisha ujuzi wa wafungwa, ambapo jumla ya wafungwa 201 wamepatiwa vyeti rasmi. Lengo la mpango huo ni kuhakikisha ujuzi walioupata Magerezani unatambulika rasmi ili kuwawezesha kupata ajira au kujiajiri mara baada ya kumaliza vifungo vyao.

Tuesday, March 18, 2025

KAMATI YA BUNGE YA AFYA NA MASUALA YA UKIMWI YAFANYA UKAGUZI ZAHANATI YA GEREZA SINGIDA.

 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya Ukimwi, ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Hassan Mtenga, imefanya ziara ya ukaguzi katika  Zahanati ya Gereza Singida, leo machi 17, 2025, ikiwa na lengo la kutathmini huduma zinazotolewa zahanati hapo.

 

Katika ukaguzi huo  Kamati ilikagua huduma za CTC, chumba  cha Maabara, chumba cha daktari, chumba cha takwimu pamoja na chumba cha  dawa,  pia  waliweza kufanya  kikao na Kamati ya mkoa ya Afya  na masuala  ya  Lishe  na kuupongeza uongozi wa  jeshi la magereza kwa huduma  wanazotoa katika zahanati hiyo.


"Hongereni kwa kazi kubwa na nzuri ambayo  mnafanya, tumejionea ,  DMO pamoja na  dactari mkuu wa mkoa  tunaomba  mtatue changamoto ndogondogo zinazokabili  zahanati ya gereza" alisema  Mhe. Mtenga


Aidha Mhe. Mtenga ametoa rai kwa Wajumbe wa Kamati hiyo pamoja na wabunge wote nchini  kujenga utamaduni wa kutembelea  Magereza mbalimbali ili kubaini changamoto zinazoyakabili na kuzitafutia ufumbuzi.


Kwaupande wake Kamishina Jenerali wa  Magereza  Jeremia  Yoram Katungu  ameishukuru  Kamati ya Bunge  ya Afya na Masuala ya  Ukimwi kwa kutembelea na kukagua Zahanati hiyo na kuahidi kuyafanyia kazi maelekezo yote waliyoyatoa ili kuboresha huduma za Afya

Monday, March 17, 2025

KAMATI YA BUNGE MAMBO YA NJE ULINZI NA USALAMA (NUU) YATEMBELEA GEREZA KUU ISANGA.


Kamati ya Bunge Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama (NUU) ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Vita Kawawa, Machi 13,2025,  wametembelea Gereza Kuu Isanga jijini Dodoma kujionea miradi mbalimbali inayoendelea katika Gereza hilo pamoja na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Gereza Maalum.


Akizungumza mara baada ya ukaguzi ujenzi wa Gereza Maalum, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Vita Rashid Kawawa ameonesha kuridhishwa na maendeleo ya ujenzi na kulipongeza Jeshi la Magereza kwa kusimamia kikamilifu Fedha za Serikali katika kutekeleza mradi.


‎Aidha Kamati hiyo imelipongeza Jeshi la Magereza kwa kutekeleza agizo la Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia vema matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwemo matumizi ya mkaa mbadala(Briquettes),Gas asili(Natural Gas) magerezani na kufanikisha kuondokana na nishati chafu. 

‎Kwa upande wake Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza (CGP) Jeremiah Katungu ameishukuru kamati hiyo kwa mafanikio aliyoyapata kwa bajeti ya mwaka 2023/24 na kufanikisha ukarabati wa Gereza maalum liliopo eneo la Gereza kuu Isanga.

‎"Jeshi linaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama kwa namna anavyoliwezesha Jeshi la Magereza katika kutekeleza majukumu yake ya msingi ikiwemo miradi ya kimaendeleo" alisema CGP. Jeremiah Katungu.

ZIARA YA NDC MAKAO MAKUU YA MAGEREZA


Wakufunzi na wanafunzi kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC),leo Machi 12,2025 wamefanya ziara Makao Makuu ya Jeshi la Magereza Msalato jijini Dodoma, lengo likiwa ni kujifunza shughuli mbalimbali zinazofanywa na Jeshi la Magereza.

Akiongea katika hotuba yake Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza (CGP)Jeremiah Yoram Katungu amekipongeza Chuo hicho kwa kufanya ziara Makao Makuu ya Jeshi la Magereza huku akisema uhusiano huo unalenga kujenga na kuimarisha katika muktadha wa kulinda mataifa yetu kuendelea.

Kwa upande wake Brigedia Jenerali C.J.Ndiege ambaye ni mkuu wa msafara kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) amesema kuwa miongoni mwa malengo ya Chuo hicho ni kutoa mafunzo ya kimkakati katika masuala ya ulinzi kwa sekta binafsi, kikanda na kimataifa.

Aidha katika ziara hiyo kulitolewa wasilisho la matumizi ya teknologia ya habari magerezani,ambapo wasilisho hilo lilitolewa na Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Kizito Jaka.


Pamoja na mambo mengine washikiri katika ziara hiyo walipata fursa ya kupanda miti eneo linalozunguka Makao Makuu ya Jeshi la Magereza.

WAZIRI BASHUNGWA ATUNUKU VYETI KWA WAFUNGWA 201 WALIOHITIMU MAFUNZO GEREZANI

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Innocent Lugha Bashungwa (Mb), leo Machi 11, 2025 amezindua Programu ya Urasimishaji wa ujuzi uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa mafunzo (Recognition of Prior Learning - RPL) na kuwatunuku vyeti vinavyo tambulika na VETA Wafungwa 201 waliohitimu Mafunzo ya fani mbalimbali yaliyotolewa na Jeshi la Magereza.


Akizungumza katika hafla hiyo ya utoaji vyeti Mhe. Bashungwa alisema Programu hiyo itatoa hamasa kwa wafungwa kujifunza na kushiriki kikamilifu katika shughuli mbalimbali za urekebishaji ili kupata ujuzi, elimu, na maarifa kwa ajili ya kuwasaidia kujiajiri au kuajiriwa pindi watakaporudi katika jamii baada ya kutumikia vifungo vyao magerezani. 


Kwaupande wake Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza (CGP) Jeremiah Yoram Katungu, ameishukuru Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi stadi (VETA) kwa kukubali kuingia makubaliano na Jeshi la Magereza na kutoa vyeti kwa Wafungwa wanohitimu fani mbalimbali Magerezani.


Hafla ya utoaji vyeti kwa Wafungwa ilifanyika Chuo KPF Mkoani Morogoro ambapo Wafungwa waliotunukiwa vyeti wamehitimu katika fani ya Umeme, Ujenzi, ufundi rangi, bomba, magari, upishi, ushonaji na Seremala.

Thursday, February 27, 2025

WAFUNGWA 118 KUNUFAIKA NA MPANGO WA PAROLE


Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Parole  Mhe. Balozi Khamis Kagasheki Feberuari 20, 2025 aliongoza kikao cha 52 cha  Bodi ya Taifa ya Parole kilichofanyika kwa muda wa siku mbili katika Ukumbi wa Corridor Springs Hotel jijini Arusha ambapo 
wajumbe wamejadili na kupendekeza wafungwa ambao wana sifa ya kunufaika na mpango wa Sheria ya Parole.

Pia Mhe. Kagasheki alisema kuwa wafungwa waliojadiliwa wameshatumikia sehemu ya kifungo chao gerezani na kifungo kilichobaki wataenda kumalizia wakiwa na familia zao na jamii kama Sheria ya Parole inavyotaka.

''Bodi imepitia kwa umakini majalada 132 na kuona kama vigezo, Kanuni, taratibu na Sheria zimefuatwa  hivyo basi Bodi imeamua kuwa wafungwa 118 wanastahili kunufaika na mpango huo wa Parole'' Alisema Kagasheki.

Kwa upande wake Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP) Jeremiah Yoram Katungu ametoa rai kwa jamii na wananchi kwa ujumla kushirikiana kwa pamoja na Jeshi la Magereza kuwapokea Wafungwa ambao wanatarajia kutoka gerezani kwa mpango wa Parole, nakusema kuwa Wafungwa hawa wamejirekebisha kitabia na mienendo yao wakiwa gerezani.

Pamoja na mambo mengine CGP Katungu alisema kuwa utaratibu wa Parole umewekwa kwa mujibu wa Sheria na umeainisha vigezo ambavyo vinatakiwa kuzingatiwa ili mfungwa aweze kunufaika na mpango huo, akivitaja vigezo hivyo ikiwemo urefu wa kifungo chake, tabia na mwenendo wake akiwa gerezani, lakini kama jamii nayo iko tayari kumpokea, hayo yote yanazingatiwa wakati Bodi inamjadili mfungwa huyo ili aweze kupendekezwa kwa utaratibu wa Parole.

Kikao hicho cha 52 cha Bodi ya Taifa ya Parole kimejadili jumla ya majalada 132, na majalada 118 yamekidhi vigezo vya mpango huo.

WAZIRI BASHUNGWA AZINDUA MABASI YA KUSAFIRISHA MAHABUSU KWENDA NA KURUDI MAHAKAMANI

 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Innocent Lugha Bashungwa, Februari 14, 2025 alifanya ziara Makao Makuu ya Jeshi la Magereza na kuzindua Mabasi Saba ya kubebea Mahabusu kwenda na kurudi Mahakamani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mabasi hayo Mhe. Bashungwa amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri na kubwa anayo endelea kuifanya ya kuboresha Jeshi la Magere

za kwa kulipatia vifaa na vitendea kazi mbalimbali ikiwemo mabasi tuliyo yazindua na kutoa wito wa kuyatunza magari hayo ili yadumu na kutoa huduma iliyokusudiwa.

"Nitumie nafasi hii kumshukuru sana Rais wetu na Amiri Jeshi Mkuu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanya yakuboresha Jeshi letu la Magereza, kuliwezesha Jeshi letu la Magereza kuwa na vifaa na vitendea kazi kama ambavyo tumeshuhudia uzinduzi wa mabasi haya ambayo yanaenda kuboresha huduma kwa ndugu zetu wafungwa" alisema Mhe. Bashungwa

Aidha,  Mhe. Bashungwa amelipongeza Jeshi la Magereza nchini kwa kutekeleza kikamilifu jukumu la kuwapa ujuzi wafungwa ikiwemo ufundi stadi na kuuendeleza ujuzi wa wafungwa wanaoingia nao, huku akieleza mkakati uliopo wa kuzindua program maalum kwa kushirikiana na VETA ili kutoa vyeti kwa wafungwa baada ya kupata ujuzi Gerezani.

Katika hatua nyingine Mhe. Bashungwa amempongeza CGP. Katungu kwa kusimamia agizo la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, la kuachana na matumizi ya kuni na kuanza kutumia nishati safi ya kupikia katika Magereza yote hapa nchini.